WARSHA YA WIKI MOJA KWA REDIO ZA JAMII NCHINI KATIKA KUTEKEKELEZA MRADI WA DEMOKRASIA NA AMANI WA UNESCO UNAOFADHILIWA NA UNDP YAMALIZIKA WILAYANI SENGEREMA

IMG_2735
Afisa Mipango Taifa wa Kitengo cha Mawasiliano na Habari na mratibu wa miradi ya UNESCO Yusuph Al-Amin asikiliza maoni wakati akiendesha mjadala wa namna ya ku-brand mradi wa Demokrasi na Amani (DEP) kuelekea uchaguzi 2015 kwa Mameneja na Wakurugenzi wa redio za jamii 25 nchini zilizohudhuria siku ya kufunga warsha ya wiki moja iliyoandaliwa na shirika la UNESCO na kufadhiliwa na UNDP.
IMG_2789
Meneja wa mradi wa Amani na Demokrasi (DEP ) kutoka UNESCO Courtney Ivins akizungumza na Mameneja na Wakurugenzi wa redio za jamii kupata tathmini ya warsha hiyo iliyomalizika mwishoni mwa Juma wilayani Sengerema mkoani Mwanza.
IMG_2743
Washiriki wakijadiliana katika makundi mambo mbalimbali ya kuboresha kwenye redio jamii zao katika utekelezaji wa mradi wa DEP kuelekea uchaguzi 2015 wakati wa kuhitimisha warsha hiyo iliyomalizika mwishoni mwa Juma.
IMG_2741
IMG_2739
Mkufunzi na Mshauri wa redio za jamii kutoka UNESCO Mama Rose Haji Mwalimu akifafanua jambo kwa Afisa Mipango Taifa wa Kitengo cha Mawasiliano na Habari na mratibu wa miradi ya UNESCO Yusuph Al-Amin wakati wa kuhitimisha warsha ya wiki moja wa redio za jamii katika kuziandaa kuendesha mijadala ya Amani na Demokrasia kuelekea uchaguzi wa mwaka 2015.
IMG_2763
Msafiri Andrew kutoka Mpanda FM akiwasilisha maoni ya kikundi chake nini kifanyike katika utekelezaji wa mradi wa Demokrasia na Amani kwa redio za jamii kuelekea uchaguzi 2015.
IMG_2718
Meneja wa Triple A FM Borry Mbaraka akichangia maoni wakati wa kufunga warsha ya wiki moja kwa Wakurugenzi na Mameneja wa Redio za jamii nchini iliyomalizika mwishoni mwa wiki wilayani Sengerema mkoani Mwanza.
IMG_2798
Meneja Mawasiliano wa Pangani FM Abdullah Mfuruki akichukua matukio mbalimbali ya kumbukumbu wakati wa kuhitimisha warsha warsha ya wiki moja iliyoandaliwa na UNESCO na kufadhiliwa na UNDP iliyowakutanisha Mameneja na Wakurugenzi wa radio za jamii 25 nchini kwa ajili ya kuwaandaa kuendesha mijadala ya Amani na Demokrasia kuelekea uchaguzi wa mwaka 2015.
IMG_2714
Sehemu ya washiriki ambao ni Mameneja na Wakurugenzi wa redio za jamii nchini waliohudhuria warsha hiyo ya wiki moja iliyomalizika mwishoni mwa Juma kwenye kituo cha Habari na Mawasiliano cha Telecentre wilayani Sengerema mkoani Mwanza iliyoandaliwa na shirika la UNESCO na kufadhiliwa na UNDP.
IMG_2813
Meneja wa Kituo cha Habari na Mawasiliano cha Telecentre SengeremaFM mkoani Mwanza Bw. Felician Ncheye akitamka kufunga rasmi warsha ya wiki moja kwa redio za jamii katika kutekeleza mradi wa Demokrasia na Amani kuelekea uchaguzi 2015.
IMG_2823
Mshauri wa Redio za Jamii kutoka UNESCO Mama Rose Haji Mwalimu akigana na Meneja wa Mradi wa DEP kutoka UNESCO Courtney Ivins mara baada ya kuhitimisha warsha ya wiki moja iliyokuwa ikifanyika kwenye kituo cha Habari na Mawasiliano cha Sengerema Telecentre mkoani Mwanza mwishoni Juma.
IMG_2825
Mameneja na Wakurugenzi wa redio za jamii nchini kwenye picha ya pamoja na wawezeshaji mara baada ya kumalizika kwa warsha ya wiki moja kwa ajili ya kuwaanda redio za jamii kuendesha mijadala ya Amani na Demokrasi kuelekea uchaguzi 2015 iliyoandaliwa na shirika la UNESCO na kufadhiliwa na UNDP.

FORTUNATA MASHINJI AHEHEREKEA SIKU YA KUZALIWA NA WAFANYAKAZI WENZAKE

 Keki ya Fortunata ambayo ilikuwa maalumu kwenye siku yake ya kuzaliwa ambayo alikula pamoja na wafanyakazi wenzake wa LAPF ,Dodoma.
 Fortunata akimlisha keki rafiki yake Scola
 Wakati wa kugonga glasi kama ishara ya kumpongeza Fortunata kwa kuongeza umri zaidi katika sherehe ndogo iliyofanyika kwennye Pub maarufu ya Ngonyani , Dodoma.
Fortunata akimimina champaigne kwa wafanyakazi wenzake wa LAPF waliojumuika nae siku ya kuzaliwa kwake iliyofanyika hivi karibuni,Dodoma.

HOTUBA YA MHE. DKT. MOHAMMED GHARIB BILAL, MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE BARAZA LA EID EL FITR, TABORA, TAREHE 9 AGOSTI 2013

Mheshimiwa Mufti wa Tanzania ,
Sheikh Issa bin Shaaban Simba;

Mheshimiwa Fatma Mwassa
Mkuu wa Mkoa wa Tabora;

Viongozi wa Dini na Madhehebu Mbalimbali;

Viongozi wa Mkoa wa Tabora na Mikoa jirani;

Katibu Mkuu wa BAKWATA;

Wajumbe wa Baraza la Ulamaa;

Viongozi Mbalimbali wa BAKWATA;

Wageni Waalikwa;

Ndugu Waumini;

Ndugu Wananchi;

Eid Mubarak!

Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma kwa kutujalia uzima,  afya njema na kutuwezesha kujumuika hapa siku ya leo kuadhimisha tukio hili  muhimu la kumalizika kwa mfungo  wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Napenda nitumie fursa hii, kutoa shukrani zangu    za   dhati   kwako   Mufti   wa Tanzania , Shekhe Issa bin Shaaban Simba na uongozi mzima wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), kwa heshima mliyonipa, kunialika kuwa mgeni rasmi katika sikukuu hii muhimu.

Aidha niwapongeze wale wote waliojaaliwa kukamilisha ibada hii adhimu, ambayo ni moja ya nguzo kuu katika imani ya dini ya Kiislamu. Kwa wale ambao hawakupata bahati hiyo, tuzidi kumwomba Mwenyezi Mungu awajalie uhai na kuwatunuku fursa hiyo siku zijazo. Rai yangu kwa mlioshiriki ibada hii muhimu ni kwamba; endelezeni mema yote mliyofanya na kuonesha   katika  kipindi chote cha mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Matendo mema yawe sehemu ya utamaduni wa maisha yetu ya kila siku katika jamii. Naamini kwa kufanya hivyo, tutakuwa tunatekeleza kwa vitendo mafundisho ya Mtume wetu Mohammad (S.A.W) na kujiwekea fungu jema duniani na akhera.

Ucha Mungu, upole, adabu, upendo, ustahimilivu na mambo yote mema mliyowatendea ndugu, jamaa na majirani zenu katika kipindi chote cha mfungo wa Ramadhani,   yadumu   na   kuwa   kielelezo  na ushahidi wa imani yenu mbele ya wanadamu wenzenu. Kwa mwislamu mwenye imani ya kweli, kuwajali wenye shida, wajane na yatima, ni ibada muhimu kwa maisha yake ya kila siku, hili halikomi baada ya kumalizika kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Endeleeni kujitoa kwa ajili ya wenye shida, salini kwa bidii na kuzingatia mafundisho yote ya Mtume wetu Mohammad (S.A.W) mliyoyapata wakati wa mfungo. Kumbukeni kuwa kumcha Mwenyezi Mungu ni msingi wa  mafanikio  yote  hapa  duniani.   Jamii  ya  watu wacha Mungu ni jamii iliyostaarabika, isiyo na chuki, mifarakano wala ugomvi, zaidi ya hayo; inatii sheria na kuheshimu mamlaka zote zilizowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mufti wa Tanzania ;
Ndugu Waumini;
Ndugu Wananchi;

HOJA MTAMBUKA: KAMA PINDA AMEFUNGULIWA KESI KWA KUSEMA 'UTAPIGWA TU', VIPI ALIYETISHIA KUMWAGA DAMU?

Na Charles Charles
KITUO cha Sheria na Haki za binadamu (LHRC) kikishirikiana na Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS), kimemfungulia mashtaka Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Kayanza Pinda kufuatia kauli aliyotoa bungeni hivi karibuni dhidi ya wakorofi wachache wanaofanya vurugu nchini, kisha wanakaidi maagizo wanayopewa na vyombo vya dola ya kukatazwa wasifanye hivyo kwa kwenda kinyume chake.

Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk. Hellen Kijo Bisimba ndiye alifungua kesi hiyo katika Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Alhamisi iliyopita huku Mkurugenzi wa Maboresho na Utetezi wa Kituo hicho, Harold Sungusia naye akimtaja Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema kwamba ni mshtakiwa wa pili.

Mashtaka hayo yanadai kuwa kauli ya Pinda inakiuka Ibara ya 13(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 inayotumika sasa, kesi ambayo LHRC na TLS wanatetewa, kuwakilishwa au kushauriwa na jopo la mawakili 20 akiwemo aliyewahi kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama cha siasa cha NCCR – Mageuzi, Dk. Ringo Tenga.

Tayari Dk. Tenga amekaririwa na gazeti moja litolewalo kila siku nchini (siyo Uhuru) akisema wamezingatia zaidi sheria na haki za msingi za binadamu huku kauli ya Pinda iliyotolewa hadharani ikizihatarisha.

Akizungumza bungeni Juni 19, mwaka huu, Waziri Mkuu aliwaonya watu wanaofanya vurugu nchini, kisha hukaidi maagizo halali wanayopewa na vyombo vya dola kwamba waache.

“…Ukifanya fujo, (halafu) umeambiwa usifanye hiki ukaamua kukaidi utapigwa tu”, alisema alipokuwa katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu yanayoulizwa kwake kila Alhamisi wakati wa vikao vya bunge na kuendelea:

“…Wote tukubaliane kwamba nchi hii tunaiendesha kwa misingi ya sheria. Sasa kama wewe umekaidi (maagizo halali ya vyombo vya dola) unaona kwamba ni imara zaidi, wewe ndiye jeuri zaidi (polisi) watakupiga tu kwa sababu hakuna namna nyingine…”

Hayo ndiyo maneno ya Pinda yaliyosababisha aburuzwe mahakamani na LHRC na TLS huku Dk. Hellen Kijo – Bisimba, mmoja kati ya wanaharakati wanaosimama kidete mara kwa mara ili kuipinga serikali na viongozi wake akisema kuwa lazima Waziri Mkuu huyo ashughulikiwe kwa kuvunja Katiba ya nchi hii.

Nawaunga mkono LHRC na TLS kwa kuthibitisha jinsi gani walivyo mstari wa mbele katika uteteaji wa sheria, kulinda Katiba na haki za Watanzania ikiwemo Ibara ya 13(1) iliyotumika kumfungulia mashtaka hayo Pinda inayosema ifuatavyo:

“Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria” (mwisho wa kunukuu).

Mbali na hiyo, Ibara ya 14 pia inaeleza kwamba “kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria”.

Nimesema ninawaunga mkono LHRC na TLS kwa kutimiza kwa vitendo wajibu wao wa kutetea Watanzania na binadamu wengine, lakini sikubaliani kwa namna zote na ubaguzi unaozingatia maslahi ya kisiasa kuwa nani afunguliwe mashtaka ama nani asiguswe kwa vile huenda tu ni mwenzao!

Kufuatia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 uliokirejesha madarakani tena Chama Cha Mapinduzi (CCM), aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk, Wilbroad Slaa alitangaza kuwa asingekubaliana na matokeo yaliyotarajiwa kutolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) akidai hayakuwa yenyewe.

Naomba ieleweke kwamba sina kinyongo naye chochote kwa kutishia kufanya hivyo maana ilikuwa haki yake, lakini nafahamu pia kuwa alikuja na madai hayo kwa sababu ya taharuki itokanayo na kuchanganyikiwa akilini.

Hakuamini kushindwa katika kinyang’anyiro hicho cha juu zaidi kuliko vyote vya kisiasa kwa kuzingatia Ibara ya 33(1) – (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alichanganyikiwa kwa sababu alikuwa amejipotosha mwenyewe na kupotoshwa kwa siku nyingi kabisa kwa kuitwa Rais mtarajiwa au Mkuu wa Nchi ajaye, Kiongozi wa Serikali na pia Amiri Jeshi Mkuu wa Tano wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama.

Katika kikao chao na waandishi wa habari siku chache tu baada ya uchaguzi huo mkuu wa mwaka 2010, Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe pamoja na Dk. Slaa kwa pamoja walitishia kuwa endapo aliyekuwa mgombea urais wa CCM, Jakaya Kikwete angetangazwa kuwa mshindi ungetokea umwagaji wa damu dhidi ya Watanzania ambao ni pamoja na watoto wasiojua lolote wala chochote.

Walisema akitangazwa kuwa rais kwa awamu ya pili, Kikwete naye asingeweza kumaliza miaka mitano akiwa madarakani, kauli inayokiuka Ibara ya 38(1) ya Katiba na Ibara ya 3(14) ya Sheria ya Uchaguzi ya Mwaka 1979 iliyofanyiwa marekebisho na kuwa Ibara ya 9(15) Mwaka 1984.

Walijua wanakiuka Ibara ya 41(6) ya Katiba ya nchi yetu na Ibara ya 5 ya Sheria Na. 20 ya Mwaka 1992 na Ibara ya 10 ya Sheria Na. 34 ya Mwaka 1994 zinazohusu Utaratibu wa Uchaguzi wa Rais.

Ndivyo pia LHRC na TLS zinavyofahamu kushinda hata mimi, lakini hazifanya lolote ama kusema chochote achilia mbali kwenda kuwafungulia mashtaka ya kuvunja Katiba ya nchi yetu kama zilivyofanya dhidi ya Pinda.

LHRC na TLS zinajua ukweli kuwa Pinda alitoa kauli ile bungeni akiwatetea Watanzania wanaofanyiwa vurugu na kikundi cha wakorofi wachache, na kwamba alifanya hivyo kwa kuzingatia Ibara ya 14 – 15(1) za Katiba na Ibara ya 6(15) ya Sheria ya Haki ya Kuishi ya Mwaka 1984.

Nimesema tokea mapema kuwa nawaunga mkono LHRC na TLS kwa kuthibitisha kwa vitendo wajibu wao wa kuwatetea Watanzania na binadamu wengine, lakini katika kesi yao dhidi ya Pinda siwaungi mkono kwa sababu naamini kabisa kwamba wanachofanya sasa ni kupotosha ukweli kuhusu vifungu hivyo vya Katiba ya nchi hii!

Siwaungi mkono kwa sababu inanituma akilini kuwa kesi hiyo imefunguliwa kwa misingi ya kisiasa zaidi, chuki zao dhidi ya CCM na juhudi za makusudi za kutaka kuwatisha viongozi wa serikali yake ili kuwatia hofu isiyokuwa na maana wala faida yoyote; na pia wanajitahidi kwa nguvu zao zote, juhudi na maarifa yao yote kuvisaidia baadhi ya vyama vya siasa hasa Chadema kwa kutumia elimu yao ya sheria.

Fikiria kwa mfano viongozi wa Chadema walivyotangaza kwamba Kikwete asingedumu madarakani kwa ile miaka yake mitano ya sasa, lakini LHRC wala TLS hawakuonekana popote kwa kusema chochote midomoni mwao ama kufanya lolote kwa namna yoyote.

Wote walibaki kimya utadhani hawakuwepo kabisa Tanzania wakati kumbe wangeweza kuwafungulia mashtaka ya kutishia maisha ya rais, kuhatarisha amani na usalama wa taifa na kutaka kuipindua serikali kabla ya mwaka 2015 kinyume cha Ibara ya 38(1) ya Katiba yetu.

Hakuna yeyote kati ya LHRC na hata TLS aliyesema wala kufanya chochote, badala yake walijifanya kwamba eti hawaangalii kabisa matangazo yoyote ya televisheni, hawasikilizi redio na hawasomi magazeti na hata mtandao wowote ule wa kijamii iwe facebook, jamii forum, google na kadhalika na kwa hiyo hakuna yeyote kati yao aliyekuwa akifahamu kitu chochote kuhusiana na vitisho hivyo vya hatari kwa nchi yetu!

Mbali na kauli hizo za kutishia umwagaji wa damu na kukiuka Katiba kwa makusudi na waziwazi, Mbowe aliwatangazia tena wananchi kwamba Tanzania isingetawalika mwaka huu wa 2013.

Alikuwa akiishinikiza serikali kuwa itekeleze matakwa ya Chadema, na kwamba isipofanya hivyo Tanzania ingeingia katika wimbi kubwa la mauaji ya halaiki, utekaji nyara au mateso mengine yoyote ili mradi chama hicho kinakidhi matakwa yake ya kisiasa.

Nashangaa kwamba kumbe kuna LHRC na TLS zinazoijua vizuri Katiba ya nchi yetu, kuiheshimu pamoja na kuizingatia sana, lakini zote hazikumfungulia mashataka Mbowe wala Dk. Slaa kwa sababu tu huenda ni viongozi wao kiitikadi.

Pamoja na kutojua nani atashinda katika kesi hiyo inayotarajiwa kusikilizwa na jopo la majaji watatu ambao bado hawajatajwa, lakini kwa hukumu yoyote nitaendelea kumuunga mkono Waziri Mkuu Pinda kuwa aliitoa kauli ile kwa ajili ya maslahi ya Watanzania wote, na pia alifanya hivyo kwa kuzingatia Ibara ya 13(1) ya Katiba ya nchi hii.

Kama LHRC au TLS wanadhani alikosea na ndiyo maana wakamfungulia mashtaka, mimi siku zote nitahoji hadi waniambie ni nani aliyekiuka haki hizo za binadamu kati ya Waziri Mkuu huyo katika upande wa kwanza na Mbowe ama Dk. Slaa katika upande wa pili.

Kama ni kweli kuwa Pinda alikiuka Ibara ya 13(1) alipokemea watu wanaofanya vurugu na kutojali wanapoonywa kwamba wakiendelea watapigwa, hakika hata iweje sikubaliani kwa namna yoyote ile na LHRC wala TLS ziliposhindwa kumfungulia mashataka Mbowe wala Dk. Slaa kwa kutishia kumwaga damu na kusema Tanzania haitatawalika mwaka 2013!

Bila kufanya hivyo hata kama Pinda atafungwa endapo atashindwa katika kesi hiyo imani yangu itaendelea kuziona LHRC na TLS kwamba zinafanya ubaguzi kwa kuangalia itikadi za kisiasa.

Nitaendelea kuzihoji kama zinaunga mkono umwagaji wa damu, vurugu na kutotii mamlaka iliyopo madarakani au zinataka Tanzania pia isitawalike kama ilivyo Iraki, Sudan, Somalia, Pakistani, Afghanistan au Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambako mauaji ya halaiki ni jambo la kawaida.

Kama LHRC na TLS zinaiona kauli ile ya Pinda aliposema ukijifanya jeuri “utapigwa tu” inakiuka Ibara ya 13(1) ya Katiba na kufunguliwa kesi; vipi Mbowe aliyetishia kumwaga damu kwa kusema Tanzania haitatawalika mwaka 2013?

Kila Mtanzania wa kweli aingie kichwani mwake na kujiuliza mwenyewe!

Mwandishi wa makala hii ni Katibu wa CCM wa Wilaya ya Shinyanga Mjini

HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWA WANANCHI, TAREHE 31 JULAI, 2013

Ndugu wananchi;
Kama ilivyo ada naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha kwa mara nyingine tena kutekeleza utaratibu wetu huu mzuri tuliojiwekea wa Rais kuzungumza na taifa kila  mwisho wa mwezi.
Ndugu Wananchi;
Mwezi Julai, 2013 ulikuwa wa neema kubwa ya wageni kwa nchi yetu wakiwemo watu na viongozi mashuhuri duniani. Natoa shukrani nyingi kwa Watanzania wenzangu kwa jinsi tulivyowapokea wageni wetu zaidi ya 1,700.  Wamefurahi kuwepo kwao nchini na wameondoka wakiwa na kumbukumbu nzuri ya nchi yetu.  Wageni wetu wamekuwa wa manufaa makubwa kwa nchi yetu.  Wamesaidia kuitangaza Tanzania duniani na kuendeleza fursa za kukuza utalii, biashara na uwekezaji nchini na kwingineko katika Afrika.
Mkutano wa Smart Partnership
Ndugu wananchi;
Wageni wetu wa kwanza ni wale waliokuja kuhudhuria Mkutano wa Global 2013 Smart Partnership Dialogue uliofanyika Dar es Salaam tarehe 28 Juni hadi 1 Julai, 2013.  Mkutano huo
ulihudhuriwa na watu zaidi ya 800 kutoka mabara yote duniani wakiwemo Watanzania.  Miongoni mwa waliohudhuria ni pamoja na wakuu wa nchi na Serikali, viongozi wastaafu, wanadiplomasia, wawakilishi wa mashirika na taasisi za kimataifa, makampuni ya ndani na nje, wafanyabiashara, wasomi, asasi za kijamii na watu wa makundi mbalimbali katika jamii.  Makampuni yetu 21 nayo yaliungana na makampuni mengine 28 kutoka nje ya nchi kushiriki kwenye maonesho ya matumizi ya sayansi na teknolojia yaliyofanyika sambamba na mkutano huo.
Ndugu Wananchi;
Agenda kuu ya majadiliano ya mwaka huu ilikuwa ni “Matumizi ya teknolojia kama nyenzo ya kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi Barani Afrika (Leveraging Technology for Africa’s Social-Economic Transformation: The Smart Partnership Way).  Tuliichagua mada hii kwa kuwa ni ukweli ulio wazi kuwa matumizi ya sayansi na teknolojia ndiyo chachu kubwa iliyoleta mageuzi na maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi. Ndiyo siri ya mafanikio katika nchi zilizoendelea na zinazopiga kasi kubwa ya maendeleo duniani.
Bahati mbaya sana kumekuwa na maendeleo na matumizi madogo ya sayansi na teknolojia katika Afrika.  Ndiyo maana nchi za Afrika ziko nyuma kimaendeleo ukilinganisha na zile zilizoendelea.  Katika mkutano huo umuhimu wa kuendeleza na kuongeza matumizi ya sayansi na teknolojia kwa ajili ya maendeleo Barani Afrika ulitambuliwa na kusisitizwa.
Mkutano ulihimiza na kusisitiza kuwa sera, mikakati na mipango ya maendeleo ya nchi za Afrika zitoe kipaumbele kwa kuendeleza matumizi ya sayansi na teknolojia.  Nchi zetu zimehimizwa kuwekeza katika elimu ya sayansi na teknolojia pamoja na kujenga uwezo wetu wa ndani wa uvumbuzi, ubunifu, umiliki na uendelezaji wa sayansi na teknolojia. Aidha, imesisitizwa kwa nchi zetu ziongeze  kasi ya kutumia sayansi na teknolojia katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii ili kuongeza ufanisi na kasi ya maendeleo.
Ndugu Wananchi;
Jambo la kutia faraja kwetu nchini ni kwamba mambo yote hayo tunayafanya.   Tunachotakiwa sasa ni kufanya vizuri zaidi na kuongeza uwekezaji na kasi ya kuendeleza matumizi ya sayansi na teknolojia katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.  Tutaendelea kuboresha sera, kuboresha mazingira ya uwekezaji na kwa ajili ya maendeleo ya sayansi na teknolojia nchini.
Ziara ya Rais wa Marekani Nchini Tanzania
Ndugu wananchi;
Mgeni wetu wa pili alikuwa Rais wa Marekani, Mheshimiwa Barack Obama, aliyefanya ziara nchini kwetu kati ya tarehe 1  - 2 Julai, 2013.  Lengo la ziara yake ilikuwa kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Marekani na Tanzania.  Kama mjuavyo, nchi zetu mbili zina uhusiano wa kibalozi tangu Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961 na Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar mwaka 1964.
Uhusiano wetu umepita katika vipindi mbalimbali na kwamba hivi sasa umekuwa mzuri zaidi kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya nchi zetu mbili.  Kumekuwepo na ongezeko kubwa la misaada ya maendeleo kutoka Marekani na uwekezaji wa vitega uchumi na biashara navyo vinakua.  Pia ziara za kiserikali za viongozi wa nchi zetu kutembeleana zimeongezeka. Kama mtakavyokumbuka, mwaka 2008 aliyekuwa Rais wa Marekani Mheshimiwa George W. Bush alifanya ziara ya siku nne nchini.  Pia Mawaziri mbalimbali wa Serikali ya Marekani wametembelea Tanzania akiwemo Mheshimiwa Hilary Clinton akiwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani aliyekuja mwaka 2011. 
Ndugu Wananchi;
Nchi ya Marekani imekuwa mshirika wetu muhimu wa maendeleo katika nyanja mbalimbali.  Kwa upande wa afya kwa mfano, tunapata msaada mkubwa katika mapambano dhidi ya malaria na UKIMWI.  Katika maendeleo ya elimu, nako wanatusaidia katika mafunzo ya wataalamu mbalimbali pamoja na upatikanaji wa vitabu vya sayansi na hisabati kwa ajili ya shule za sekondari.  Kupitia Mfuko wa Changamoto za Milenia, Marekani inatusaidia katika kuimarisha miundomuinu ya barabara, umeme na maji.  Ujenzi wa barabara za Tanga – Horohoro, Namtumbo – Songea – Mbinga; Tunduma – Sumbawanga na baadhi ya barabara za Pemba, ujenzi wa njia ya pili ya kupeleka umeme Unguja kutoka Dar es Salaam, ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mafia na usambazaji wa umeme katika Mikoa 10 ya Tanzania bara ni miongoni mwa matunda ya msaada wa Mfuko huo.  Pamoja na hayo, ipo miradi ya kuongeza maji katika jiji la Dar es Salaam na Manispaa ya Morogoro ambayo inaendelea kutekelezwa.
Ndugu Wananchi;
Wakati wa ziara yake, Rais Obama alielezea na kusisitiza dhamira yake na ya Serikali yake ya kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya nchi zetu.  Alielezea kuridhika na hatua tuliyofikia ya kukuza demokrasia nchini, utawala bora na kuwekeza katika maendeleo ya watu wetu.  Aliahidi kuendelea kuunga mkono juhudi zetu.  Katika hili ameahidi kuongeza misaada ya maendeleo na kiufundi katika sekta za afya, elimu, kilimo, barabara, nishati na maendeleo ya vijana.  Pia, alithibitisha kwamba nchi yetu itaendelea kunufaika na ufadhili wa Awamu ya Pili ya Mfuko wa Changamoto za Millenia.  Katika awamu hii, maeneo yatakayopewa kipaumbele hapa kwetu ni umeme na barabara za vijijini.  Mazungumzo ya miradi itakayotekelezwa katika awamu hiyo yanaendelea vizuri.
Power Africa
Ndugu Wananchi;
Rais Obama alitumia fursa ya ziara yake nchini kuzindua mpango wa Serikali yake wa kusaidia maendeleo ya sekta ya umeme katika Bara la Afrika.  Mpango huu unaoitwa “Power Africa Initiative” umetengewa kiasi cha dola za Marekani bilioni 7 na Serikali ya Marekani na makampuni binafsi ya nchi hiyo yameahidi kuwekeza dola bilioni 9 katika mpango huo.  Kwa kuanzia, nchi sita za Afrika (Ethiopia, Ghana, Nigeria, Tanzania, Liberia na Kenya) ikiwemo Tanzania zitahusishwa.
Bila ya shaka Mpango huo ukikamilika utasaidia sana kuimarisha upatikanaji wa umeme barani Afrika ambayo ni nyenzo muhimu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii.  Ni ukweli ulio wazi kuwa ukosefu wa umeme wa kutosha na wa uhakika ni sababu kubwa inayokwamisha maendeleo ya haraka katika nchi za Afrika.  Hivyo basi, msaada huu ni muhimu sana kwetu.   Kwa ajili hiyo nimeagiza Wizara ya Nishati na Madini iandae mkakati madhubuti wa namna Tanzania itakavyoshiriki na kufaidika na mpango huo.  Nataka mpango huo utakapoanza kutekelezwa utukute sisi tupo tayari kutumia fursa zake.
Vile vile, ndugu wananchi, katika ziara hiyo Rais Obama alielezea nia ya Serikali yake kutaka kuwepo mpango wa kukuza ushirikiano wa biashara na uwekezaji baina ya nchi yake na nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.  Nimeelekeza Wizara husika yaani Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko nao watengeneze mkakati utakaoonesha jinsi tulivyojipanga kufaidika na mpango huo.  Lazima tujiandae vyema na mapema tunufaike saiwa na mpango huo.
Ziara ya Rais Mstaafu wa Marekani Nchini
Ndugu Wananchi;
Sambamba na ziara ya Rais Obama, nchi yetu ilipata bahati ya kutembelewa tena na Rais Mstaafu wa Marekani, Mheshimiwa George W. Bush na mkewe Laura Bush, tarehe 1 hadi 3 Julai, 2013.  Kwa udhamini wa asasi ya George W. Bush Foundation waliandaa Mkutano wa Wake wa Marais wa Afrika uliofanyika hapa Dar es Salaam, tarehe 2 na 3 Julai, 2013.  Mama Michelle Obama naye alishiriki mkutano huo uliozungumzia kuimarisha maendeleo na afya ya wanawake Barani Afrika.
Katika mkutano huo, pia, Mheshimiwa George W. Bush alizindua mpango wa kuimarisha mapambano dhidi ya kansa ya shingo ya kizazi na matiti barani Afrika.  Kufuatia Mpango huo, Serikali ya Marekani imetoa dola milioni 3 na mashine 16 za Cryo Therapy zinazotumia baridi kali kuua chembechembe za kansa.  Msaada huo ni muhimu hasa ukizingatia kuwa kila mwaka hapa nchini zaidi ya Watanzania 21,000 wanapata maradhi ya kansa.  Kati ya hao asilimia 29.4  ni wanawake wanaopata magonjwa ya kansa ya shingo ya uzazi na asilimia 6.2 wanapata kansa ya matiti. Naamini Mpango huu utatusaidia sana katika kuimarisha mapambano dhidi ya maradhi haya yanayowasumbua na kuua kina mama wengi nchini.  Nimeitaka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuweka utaratibu mzuri ili msaada huo utumike ipasavyo na kuwanufaisha walengwa.
Ziara ya Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza Nchini
Ndugu Wananchi;
Tarehe 23 mwezi Julai, 2013 pia tulitembelewa na Waziri Mkuu Mstaafu wa Uingereza, Mheshimiwa Tony Blair.  Katika mazungumzo yetu Mheshimiwa Blair aliahidi kuisaidia nchi yetu kupitia taasisi yake ya Africa Governance Initiative kusaidia kusambaza umeme wa jua katika shule zetu za sekondari vijijini, maboresho ya shirika letu la umeme (TANESCO) na kusaidia uanzishaji na uimarishaji wa Kitengo cha Rais cha Ufuatiliaji Utekelezaji wa Programu za Maendeleo (Presidential Delivery Bureau - PDB).   Tunamshukuru kwa ahadi yake hiyo itakayochangia katika jitihada za kujiletea maendeleo. 
Ziara ya Waziri Mkuu wa Thailand Nchini
Ndugu Wananchi;
Tarehe 30 Julai, 2013 tulimpokea Mheshimiwa Yingluck Shinawatra, Waziri Mkuu wa Thailand aliyefanya ziara ya siku tatu nchini.  Lengo la ziara yake ni kuimarisha uhusiano mzuri uliopo kati ya Thailand na Tanzania. Katika ziara hiyo, tumezindua Jukwaa la Wafanyabiashara wa Thailand na Tanzania (Thai-Tanzania Business Forum) ili kukuza biashara na uwekezaji baina ya nchi zetu.  Waziri Mkuu Yingluck Shinawatra alitumia fursa hiyo kufafanua sera ya Thailand kwa Afrika inayosisitiza kukuza ushirikiano wa karibu wa kiuchumi na kibiashara.  Pia amepata nafasi ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kujionea mwenyewe jinsi nchi yetu ilivyobarikiwa kwa kuwa na kivutio hicho cha aina yake.  Alipokuwa kule nchi zetu zilitiliana saini maelewano ya ushirikiano katika kulinda na kuhifadhi wanyama pori.
Katika mazungumzo yangu na yeye, tumekubaliana kuchukua hatua thabiti kukuza ushirikiano katika nyanja mbalimbali.  Tumetiliana saini mikataba mitano ya ushirikiano kwa mambo yafuatayo:  Kukuza na kulinda vitega uchumi; kubadilishana wafungwa; ushirikiano wa kiufundi; na ushirikiano kwa masuala ya madini. Aidha, Waziri Mkuu huyo ameahidi kuwahimiza wawekezaji wa nchini mwake kuja Tanzania kuwekeza katika sekta mbalimbali za uchumi ikiwemo kilimo, utalii, viwanda nakadhalika.          Pia, Waziri Mkuu wa Thailand ameahidi kuwa Serikali yake itatoa ufadhili kwa vijana 10 kusoma Shahada ya Uzamili nchini humo.  Vile vile, nchi hiyo itaanza kuleta wataalamu wa afya wa kujitolea kuja kushirikiana na wataalam wetu kuimarisha huduma ya afya nchini. 
Ziara hizi zinaonesha utayari wa dunia kuunga mkono jitihada zetu za kujiletea maendeleo.  Naomba Watanzania wenzangu tutumie vizuri utayari huo wa dunia kuongeza kasi ya maendeleo yetu.  Tusijikwaze wenyewe.
Ziara ya Kagera
Ndugu wananchi;
Kuanzia tarehe 24 hadi 29 Julai, 2013, nilifanya ziara Mkoani Kagera.  Nilishiriki kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa na kuzindua jengo jipya la Mahakama Kuu. Pia niliweka jiwe la msingi la upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Bukoba na kuweka mawe ya msingi ya ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara za Kigoma – Lusahunga na Kyaka – Kayanga – Bugene.  Vile vile nilizindua Wilaya mpya ya Kyerwa na kukagua shughuli za maendeleo pamoja na kuona na kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi ili kuzitafutia majawabu.
Sherehe za Kumbukumbu ya Mashujaa zilifana sana.   Niliwapongeza viongozi wa Jeshi na wa Mkoa kwa maandalizi mazuri ya sherehe hizo.  Pia nilirudia kumpongeza Mkuu wa Majeshi, Jenerali Davis Mwamunyange, kwa uamuzi wake wa busara wa kufanya sherehe za kumbukumbu za mashujaa wetu pale Kaboya badala ya kufanyikia Dar es Salaam tu kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.  Ni uamuzi muafaka na wa busara kwani pale Kaboya ndipo walipolala  mashujaa wetu waliopoteza maisha yao kutetea mipaka na uhuru wa nchi yetu dhidi ya Nduli Iddi Amin.  Hali kadhalika, kule Naliendele, Mtwara ambapo sherehe za mashujaa zilifanyika mwaka wa juzi, ndipo walipozikwa mashujaa wetu waliopoteza maisha kuisaidia nchi jirani na rafiki ya Msumbuji kutetea Uhuru wake dhidi ya wakoloni, makaburu na vibaraka wao wa ndani ya Msumbiji.
Ndugu Wananchi;
Katika hotuba yangu pale Kaboya niliwakumbusha Watanzania wenzangu kwamba katika kuwakumbuka mashujaa wetu wale na sisi tulio hai, hatuna budi kutambua wajibu wetu wa kuwa tayari kujitolea muhanga kwa ajili ya kulinda uhuru wa mipaka ya nchi yetu.  Nilisisitiza utayari wa nchi yetu kulinda mipaka yake na kwamba mfano wa mashujaa waliolala pale ni fundisho kwa mtu ye yote anayetamani kumega kipande cho chote cha ardhi ya nchi yetu.  Atakiona cha mtema kuni kilichomkuta Nduli Iddi Amini  au hata zaidi.
Nimesikia kuwa kauli yangu ile imetafsiriwa visivyo na kupotoshwa na baadhi vyombo vya habari na hata majirani zetu.  Tafsiri hizo ni potofu.  Sikumtaja mtu ye yote au nchi yo yote.  Nilikuwa nazungumzia wajibu wa majeshi yetu na raia wa nchi yetu wa kulinda uhuru na mipaka yetu na kwamba hatutamruhusu mtu au nchi yo yote kutupokonya wala kuichezea haki yetu hiyo ya msingi.  Tuko tayari kuitetea hata kama gharama yake ni maisha yetu kama walivyofanya mashujaa waliolala Kaboya.
Mahakama Kuu
Ndugu Wananchi;
Katika ufunguzi wa Mahakama Kuu ya Bukoba nilisisitiza dhamira na utayari wa Serikali yetu kuiwezesha Mahakama ya Tanzania kuwa na Mahakama Kuu katika kila Mkoa.  Baada ya kukamilika kwa Mahakama Kuu ya Bukoba bado kuna Mikoa 14 hainazo.  Katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/14 tumetenga fedha za kujenga Mahakama Kuu katika Mikoa 7 na nilirudia ahadi yangu kuwa katika mwaka ujao wa fedha tutatoa fedha za kumalizia Mikoa 7 iliyosalia.  Niliamua tuongeze kasi ya kujenga Mahakama Kuu hizo ili kuiwezesha Mahakama ya Tanzania kutimiza ipasavyo wajibu wake wa kutoa haki nchini.
Maendeleo ya Mkoa wa Kagera
Ndugu Wananchi;
Nilipokuwa Kagera nilifurahishwa na utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo ya kiuchumi na kijamii.  Taarifa za Mkoa na Wilaya zimefafanua kwa kina mambo mazuri yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika Mkoani.  Wameelezea furaha yao kwa mafanikio yaliyopatikana ambayo baadhi nimeyashuhudia au hata kushiriki kuyazindua na kuweka mawe ya msingi.  Taarifa hizo pia zimelezea mambo mengi zaidi wanayotaka yafanyike na matatizo mapya na hata ya zamani ambayo wanataka yapatiwe ufumbuzi.
Katika mazungumzo yangu na viongozi na wananchi, yapo mambo ambayo yako kwenye uwezo wao kijijini, Wilayani na Mkoani kuyapatia ufumbuzi.  Tulikubaliana na kuelekezana nini kifanyike.  Yapo mengine mengine ambayo yanahitaji nguvu ya taifa tumeyachukua kuja kuyafanyia kazi.  Kuna baadhi yaliwahusu Mawaziri ambao nilikuwa nao ziarani waliyasemea na kuyafanyia kazi palepale yalipojitokeza.
Ulinzi na Usalama
Ndugu Wananchi;
Kuna mambo matatu yahusuyo usalama ambayo yalizungumzwa na wananchi kwa uchungu mkubwa ambayo niliamua tuyashughulikie kitaifa.  Mambo hayo ni ujambazi wa kutumia silaha kuteka magari, kupora mali na watu kuuawa.  Jambo la pili ni wahamiaji kutoka nchi jirani wanaoingia, kuishi na kufanya shughuli nchini kinyume cha sheria.   Na tatu, mifugo kuingizwa kwa wingi nchini bila kufuata taratibu husika na mingine kuingizwa katika hifadhi za wanyama.
Ndugu wananchi;
Nilitoa maagizo kwa wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama yaani JWTZ, Polisi, Usalama wa Taifa na Uhamiaji watengeneze mpango kabambe wa kuyashughulikia matatizo hayo.  Watayarishe na kutekeleza operesheni maalum itakayo au zitakazokomesha ujambazi, kuondoa wahamiaji wasiokuwa halali na kuondoa mifugo iliyoingizwa nchini kinyume na utaratibu na ile iliyoko kwenye maeneo yasiyo stahili.
Aidha, niliwataka majambazi wajisalimishe na wasalimishe silaha zao ndani ya wiki mbili na siku hizo zinaanzia tarehe 29 Julai, 2013 nilipomaliza ziara yangu Mkoani humo.  Kwa wahamiaji wanaoishi nchini kinyume cha sheria nimewataka watumie muda huo kuondoka nchini au kuhalalisha ukaazi wao.  Hivyo hivyo kwa mifugo iliyoingizwa nchini kinyume na sheria au ile iliyoko kwenye maeneo yasiyostahili.  Ndani ya muda huo watu wote waondoe mifugo yao au wajitokeze kufuata taratibu zilizopo.
Ndugu Wananchi;
Nilisema nilipokuwa Mkoani Kagera na narudia tena leo kuwa baada ya siku 14 kupita, vyombo vya ulinzi na usalama vitaendesha operesheni maalum ya kushughulikia matatizo hayo.  Nilisema kuwa operesheni hiyo itafanyika katika Mikoa ya Kigoma, Kagera na Geita kwa wakati mmoja.  Napenda kuwahakikishia kuwa hapatakuwa na mahali pa kukimbilia wala kujificha.  Nawashauri wale wote wanaohusika na ujambazi, uhamiaji haramu na uingizaji haramu wa mifugo waamue kuchukua hatua muafaka sasa.  Wasisubiri operesheni iwakute, wala wasifikirie kuwa hili ni jambo la kupita.  Safari hii itakuwa endelevu.
Ndugu Zangu;
Hatuwezi kukubali hali hii niliyoikuta Mkoani Kagera ikaachwa kuendelea.  Italeta madhara makubwa zaidi siku za usoni.  Haiwezekani raia katika nchi yake, akose uhuru na usalama wa kutembea peke yake mpaka asindikizwe na Polisi.  Na, baya zaidi hata Polisi nao wanashambuliwa na kuuawa watakavyo majambazi.  Uhalifu huu lazima ukomeshwe, uishe na usijirudie tena.
Pia, haiwezekani hali ya watu kutoka nchi jirani kuingia nchini, kuishi na kufanya shughuli na kutoka watakavyo.  Hatuzuii watu kuingia na kuishi Tanzania lakini wafuate sheria na taratibu za kuhamia na kuishi katika nchi yetu.  Nchi yetu ina sifa na ukarimu huo. Hakuna uthibitisho mkubwa zaidi ya ule wa mwaka 1982, Rais Julius Nyerere wakati ule alipowaruhusu wakimbizi wanaopenda kuwa raia wa Tanzania wafanye hivyo.  Wakimbizi 30,000 tu waliitumia fursa hiyo.  Mwaka 2010 tuliwapa uraia wakimbizi 160,000 wa kutoka Burundi. Kwa sababu hiyo hatuoni sababu ya watu kufanya wanayoyafanya sasa kule Mkoani Kagera.  Hatuwezi kuacha hali hiyo iendelee ilivyo.
Ndugu Wananchi;
Nilipokuwa Mkoani Kagera nilielezea kusikitishwa kwangu na vitendo vya baadhi ya watendaji na viongozi wa vijiji na wananchi kuwaruhusu watu kuingia na kuishi nchini kinyume cha sheria.  Nimewataka waache mtindo huo.  Nimeagiza na wao wajumuishwe katika operesheni ijayo.  Watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo haramu wachukuliwe hatua zipasazo kisheria.  Aidha, niliwataka Maafisa wa Uhamiaji watimize ipasavyo wajibu wao.  Ukweli ni kwamba, mambo haya kuendelea kwa muda mrefu kiasi hiki ni kwa sababu ya udhaifu wa mamlaka husika.  Vile vile, nimewataka TAKUKURU nao watimize wajibu wao.  Hapa kuna uthibitisho tosha wa kuwepo kwa vitendo vya rushwa vinavyohusisha wahamiaji hao na maofisa wa vijiji na idara husika za Serikali.  Mimi naamini kama TAKUKURU ikiwabana na Uhamiaji wakichemka vya kutosha tatizo hili lingepungua sana au hata kutokuwepo kabisa.
Uhusiano na Nchi ya Rwanda
Ndugu wananchi;
Katika kipindi cha miezi miwili sasa hususan tangu mwishoni mwa mwezi Mei, 2013, uhusiano baina ya nchi yetu na Rwanda unapitia katika wakati mgumu.  Kauli za viongozi wa Rwanda dhidi yangu na nchi yetu ni ushahidi wa kuwepo hali hiyo.  Napenda kuwahakikishia Watanzania wenzangu na ndugu zetu wa Rwanda kuwa mimi, Serikali ninayoiongoza na wananchi wa Tanzania tunapenda kuwa na uhusiano mzuri na ushirikiano wa karibu na Rwanda kama ilivyo kwa nchi zote jirani.  Kama majirani kila mmoja anamuhitaji mwenzake, hivyo lazima tuwe na uhusiano mwema na ushirikiano mzuri.
Napenda kusisitiza kuwa mimi na Serikali ninayoiongoza tutakuwa wa mwisho kufanya kitendo au vitendo vibaya dhidi ya Rwanda au nchi yo yote jirani au yo yote duniani.  Hatuna sababu ya kufanya hivyo kwani ni mambo ambayo hayana tija wala maslahi kwetu.
Ndugu Wananchi;
Ukweli ni kwamba wakati wote tumekuwa tunajihusisha na mambo ya kukuza na kujenga ujirani mwema na kufanya mambo ambayo yatasaidia kuimarisha uhusiano wetu kwa maslahi ya nchi zetu.  Hiyo ni moja ya nguzo kuu ya Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania. Huo ndiyo ukweli kuhusu uhusiano wetu na nchi ya Rwanda kabla na hata baada ya sintofahamu iliyojitokeza sasa.  Napenda kuwahakikishia ndugu zetu wa Rwanda kuwa kwa upande wetu hakuna kilichobadilika wala kupungua katika uhusiano na ushirikiano wetu. Mambo yapo vile vile. Kwa upande wangu, binafsi, sijasema lo lote kuhusu Rwanda pamoja na maneno mengi ya matusi na kejeli yanayotoka kwenye vinywa vya viongozi wa Rwanda dhidi yangu.  Siyo kwamba siambiwi yanayosemwa au sijui kusema au sina la kusema, la hasha.  Sijafanya hivyo kwa sababu sioni faida yake.  Kwangu mimi sioni kama kuna mgogoro wa aina yo yote.   Busara inatuelekeza kuwa tusikuze mgogoro usiokuwepo.  Waingereza wanasema “two wrongs do not make a right”.
Ndugu Wananchi;
Kama mjuavyo uhusiano wetu na Rwanda umekuwa mzuri kwa miaka mingi.  Tunashirikiana na kusaidiana kwa mambo mengi baina ya nchi zetu kitaifa na katika kanda yetu ya Afrika Mashariki na Nchi za Maziwa Makuu, katika Umoja wa Afrika na hata kimataifa.  Uhusiano unaelekea kupata mtikisiko baada ya mimi kutoa ushauri kwa Serikali ya Rwanda kuzungumza na mahasimu wao.  Ushauri ule niliutoa kwa nia njema kabisa kwani bado naamini kuwa kama jambo linaweza kumalizwa kwa njia ya mazungumzo njia hiyo ni vyema itumike.  Isitoshe, ushauri ule niliutoa pia kwa Serikali ya Kongo na kwa Serikali ya Uganda.  Katika mkutano ule Rais Yoweri Museveni wa Uganda aliunga mkono kauli yangu. Rais wa Rwanda hakusema cho chote pale mkutanoni.  Baada ya kurudi nyumbani ndipo tukaanza kuyasikia maneno tuliyoyasikia na tunayoendelea kuyasikia.
Kwa kweli nimestaajabu sana na jinsi walivyouchukulia ushauri wangu na wanayoyafanya.  Havifanani kabisa, completely out of proportion and out of context. Mimi nilifanya vile kwa kuzingatia mila na desturi zetu za miaka mingi katika ukanda wetu.  Tumekuwa tunakutana katika mikutano na vikao mbalimbali tunazungumza na kushauriana kwa uwazi juu ya njia za kushughulikia matatizo na masuala mbalimbali kila yanapotokea.  Wakati wote tumeyachukulia kuwa ni mambo yanayotuhusu sote hivyo kupeana ushauri ni wajibu wetu wote.  Na mara nyingi ushauri kwa wanaogombana kuzungumza tunautumia sana.  Iweje leo mtu kutoa ushauri ule lionekane jambo baya na la ajabu.  Jambo la kushutumiwa na kutukanwa!  Siyo sawa hata kidogo!! Ushauri si shuruti, ushauri si amri.  Una hiyari ya kuukubali au kuukataa.  Muungwana hujibu:  “Siuafiki ushauri wako”.  Hakuna haja ya kutukana wala kusema maneno yasiyostahili wala kusema yasiyokuwepo na ya uongo.
Ndugu Wananchi;
Napenda kurudia kusema kuwa mimi binafsi na Serikali yetu ya Tanzania hatuna ugomvi wala nia yo yote mbaya na Rwanda.  Tunapenda tuendelee kuwa na uhusiano mzuri na Rwanda.  Labda wenzetu wanalo lao jambo dhidi yetu ambalo sisi hatulijui.  Maana na sisi tunasikia mengi yanayozungumzwa na kudaiwa kupangwa kufanywa na Rwanda dhidi yangu na nchi yetu.  Hatupendi kuyaamini moja kwa moja tunayoyasikia lakini hatuyapuuzi.
Ndugu Wananchi;
Kabla ya kumaliza, naomba kutumia nafasi hii pia kuwatakia Waislamu wote nchini heri na baraka tele katika kukamilisha ibada muhimu ya kufunga mwezi Mtukufu wa Ramadhan.  Naomba tuendelee kuwatakia heri ili wamalize salama na tuweze kusherehekea kwa furaha na bashasha tele siku kuu ya Idd el Fitr pindi itakapowadia.
Mwisho kabisa, nawaomba Watanzania wenzangu wote tuendelee kushirikiana na kuishi kwa upendo, umoja na mshikamano kama ilivyo kawaida yetu.

Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Ibariki Afrika!

Asanteni Sana Kwa Kunisikiliza.